SHERIA NA MISINGI YETU

Katiba na Kanuni za SMART FRIENDS

Kabla ya kujiunga, soma na uelewe haki zako, wajibu wako, na jinsi kikundi kinavyofanya kazi — kwa uwazi kamili. Hakuna kufichwa.

Jiunge Nasi Leo Rudi Mwanzo
SEHEMU A
Kanuni za Uanachama na Hisa
8 Vifungu
A.1 — Hisa za Kuanza na Mwanachama Mpya
K-001 Uanachama unaanza kwa kulipa Hisa za Kianzio — sasa ni Hisa 6 × TSh 50,000 = TSh 300,000. Hizi si ada ya kiingilio bali ni Hisa za kwanza za mwanachama. Mwombaji ana siku 28 tu kulipa kwa mkupuo mmoja. Siku 28 zikipita bila malipo, nafasi inabatilishwa.
K-002 Mwombaji aliyepitishwa anapewa nafasi wazi ya siku 28 kulipa Hisa za Kuanza kamili. Ikiwa hajalipa ndani ya siku 28, nafasi yake inafutika na atalazimika kuomba upya. Idadi ya Hisa za Kuanza inaweza kubadilishwa na Mkutano Mkuu kwa 75%.
K-003 Wanachama waanzilishi 10 wote wana Hisa 6 za kuanza kila mmoja (TSh 300,000 kila mtu) kuanzia 28 Machi 2026.
A.1b — Kanuni ya Kura Moja (One Member, One Vote)
K-004 Kila mwanachama hai ana kura moja (1) tu katika maamuzi yote ya kikundi — bila kujali idadi ya Hisa zake. Mwenye Hisa 6 na mwenye Hisa 100 wana nguvu moja sawa ya maamuzi. Hisa zinatumika kwa Gawio na dhamana tu.
K-005 Vikwazo pekee vya kupiga kura: (a) mwanachama kuwa katika kipindi cha majaribio (miezi 3 ya kwanza), (b) kusimamishwa rasmi, au (c) kuwa na ukinzani wa maslahi katika jambo linalopigiwa kura.
A.2 — Hisa za Kila Mwezi
K-017 Kila mwanachama atachangia angalau Hisa mbili (2) kila mwezi (= TSh 100,000 kwa sasa). Mwanachama anaweza kuweka Hisa zaidi bila kikwazo.
K-006 Hisa zote zimegawanywa 50/50: 50% ni Hisa Huru (dhamana ya mkopo wa mwanachama), 50% ni Hisa za Uwekezaji (uwekezaji wa pamoja — HAZIINGII kama dhamana ya mkopo wa mtu).
K-007 Hisa za Uwekezaji (50%) HAZIWEZI kutumika kama dhamana ya mkopo wa mtu yeyote. Ni nguzo ya ukuaji wa pamoja wa kikundi.
K-008 Tarehe ya mwisho ya michango yote ni siku ya 28 ya kila mwezi. Malipo yanayofika baada ya tarehe hii yatachomeka faini ya 20% mara moja.
A.3 — Ada ya Uendeshaji
K-009 Kila mwezi mwanachama atalipa Ada ya Uendeshaji wakati wa kulipa Hisa zake. Kiwango kitaamuliwa na Mkutano Mkuu kwa kura nyingi.
K-010 Ada ya Uendeshaji itaingizwa kwenye mfuko wa uendeshaji peke yake — tofauti kabisa na mfuko wa Hisa na uwekezaji. Haihesabiwi kama Hisa wala hairudishwi.
K-011 Mhasibu Mkuu atatoa ripoti ya matumizi ya mfuko wa uendeshaji kila robo mwaka.
A.4 — Sifa za Mwanachama Hai
K-012 Mwanachama anaitwa "Hai" anapokidhi SIFA ZOTE: (a) anachangia Hisa 2+ kila mwezi bila kukosa zaidi ya miezi 2; (b) analipa Ada ya Uendeshaji; (c) hana malimbikizo ya faini; (d) anahudhuria vikao; (e) ameweka taarifa ya mrithi wake.
K-013 Mwanachama "Si Hai" hatapiga kura katika maamuzi ya fedha au kiuongozi, wala kugombea nafasi — hadi sifa zake zirejeshewe.
K-014 Kila mwanachama LAZIMA asajili mrithi wa kisheria kwa Katibu ndani ya miezi 2 ya kujiunga.
K-015 Mwombaji wa uanachama lazima aletwe na Mwanachama Mhakikishaji — mwanachama hai anayemjua vizuri, si tu kujuana tu.
K-016 Wajibu wa Mhakikishaji: ikiwa mwanachama aliyemhakikishia ataonekana na dosari ya maadili au udanganyifu ndani ya mwaka mmoja, Mhakikishaji atapitiwa na uongozi.
A.5 — Mahudhurio
K-017b Mahudhurio ya vikao ni wajibu wa uanachama, si hiari. Mwanachama asiyeweza kuhudhuria atatoa taarifa kwa Katibu kabla ya kikao.
K-018 Kutokuhudhuria bila taarifa inayokubaliwa = faini ya TSh 20,000 inayokatwa moja kwa moja kwenye Hisa. Kutokuhudhuria vikao 3 mfululizo bila sababu = suala linashughulikiwa na uongozi.
A.6 — Tabia Katika Vikao
K-019 Kila mzungumzaji ataomba ruhusa kwa Mwenyekiti. Lugha ya vikao: Kiswahili. Simu za mkononi: lazima ziwe kimya (silent) ndani ya kikao.
K-020 Uamuzi wowote uliofikiwa kwa akidi inayohitajika ni wa mwisho kwa kikao hicho. Hauwezi kufunguliwa tena bila mchakato rasmi wa mabadiliko.
A.3b — Mchango Maalumu (Special Levy)
K-021 Mchango Maalumu HAUKUKUSANYIKI bila: (1) Pendekezo rasmi la maandishi, (2) Taarifa kwa wanachama WOTE si chini ya siku 14, (3) Kikao chenye akidi kamili, (4) Kura ya 2/3 ya wanachama WOTE, (5) Kumbukumbu rasmi kwenye minutes. Mwanachama ana haki ya KUKATAA bila adhabu.
SEHEMU B
Kanuni za Fedha
4 Vifungu
B.1 — Akaunti Mbili za Kikundi
B.1a SMART FRIENDS Mkoba: akaunti ya simu ya mkoba (M-Pesa au iliyoidhinishwa) — miamala ya kila siku: Hisa, mikopo, marejesho, riba, faini, Ada ya Uendeshaji.
B.1b Akaunti ya Benki: hifadhi kuu ya mtaji mkubwa wa Hisa na Uwekezaji. Inatumika kwa uhifadhi wa muda mrefu. Inahitaji saini za watia saini watatu.
B.1c Fedha zote za kikundi, iwe Hisa, riba, faini, au mapato ya uwekezaji, zinapita kwenye Mkoba au Akaunti ya Benki — HAZIWEZI kukaa kwa kiongozi yeyote binafsi.
B.2 — Mfumo wa Idhini ya Malipo (Mkoba)
Daraja 1 Hadi TSh 50,000: Mhazina Msaidizi peke yake (kwa kibali cha maandishi/dijitali kinachohifadhiwa).
Daraja 2 TSh 50,001–200,000: Mhasibu Mkuu au Mhazina Msaidizi + idhini ya Katibu au Mwenyekiti (ujumbe rasmi unaohifadhiwa).
Daraja 3 Zaidi ya TSh 200,000: Lazima iwe na uamuzi wa Bodi ya Uongozi (Mwenyekiti + Mhasibu + Katibu, wanachama 3+ wa bodi).
B.5 — Faini Inayokusanyika
B.5a Faini ya 20% inaongezwa mara moja baada ya kukosa tarehe ya 28. Kisha inaendelea kuongezeka kwa 20% ya jumla ya deni kila mwezi unaopita bila malipo.
B.5b Faini inakatwa moja kwa moja kutoka akiba (Hisa) ya mwanachama na mwanachama anapata arifa ya mara moja kupitia mfumo.
B.5c Mwanachama mwenye faini isiyolipwa HAWEZI kupata mkopo mpya hadi faini imelipwa.
B.6 — Gawio
B.6a Gawio linatokana na: riba za mikopo yote yaliyolipwa, mapato yote ya uwekezaji wa pamoja, na faini zote zilizokusanywa.
B.6b Gawio linagawanywa kwa wanachama WOTE WALIOPO wakati wa ugawaji kwa uwiano wa Hisa zao ZOTE (Hisa Huru + Hisa za Uwekezaji). Mwanachama aliyeacha kikundi kabla ya ugawaji hapati Gawio la kipindi hicho.
B.6c Hasara ya uwekezaji inagawanywa kwa wanachama wote kwa uwiano wa Hisa zao — kama vile Gawio. Hasara inakatwa kwanza kutoka mfuko wa Gawio uliokusanyika kabla ya kuathiri Hisa za wanachama.
SEHEMU C
Kanuni za Mikopo
4 Vifungu
C.1 — Kamati ya Mikopo
C.1a Wanachama watatu (3) wasio uongozi wanaochaguliwa na Mkutano Mkuu kila mwaka ndio Kamati ya Mikopo. Wao peke yao wana mamlaka ya kupitisha au kukataa maombi yote ya mikopo.
C.1b Uamuzi wa Kamati ya Mikopo utatolewa ndani ya SAA 24 za ombi kupokewa. Ombi lolote lililokaa zaidi ya SAA 24 bila uamuzi linachukuliwa kuwa limepitishwa kwa muda — na Kamati inatakiwa kueleza sababu ya kuchelewa.
C.1c Uamuzi wa kupitisha au kukataa mkopo HAUWEZI kupingwa na kiongozi mmoja au Mwenyekiti — lazima ufuate mchakato wa ombi la upya kwa Kamati.
C.2 — Kanuni ya Msingi: Hisa Huru 100%
C.2a Kiwango cha juu cha mkopo: 100% ya Hisa Huru za mwanachama (50% ya Hisa zake ZOTE). Mfano: Hisa 12 × TSh 50,000 = TSh 600,000 → Hisa Huru = TSh 300,000 → mkopo wa juu = TSh 300,000.
C.2b Mwanachama aliye na mkopo unaoendelea hawezi kupata mkopo mwingine MPAKA mkopo wa kwanza umelipwa kabisa.
C.2c Mwanachama mwenye faini isiyolipwa, deni la mwezi wa Ada, au malimbikizo yoyote HAWEZI kupata mkopo mpya hadi deni lote limelipwa.
C.2d Mkopo unalipwa ndani ya miezi mitatu (3) ya kupewa, kwa awamu za kila mwezi zinazolingana na mapato ya mkopaji — zilizopangwa na Kamati ya Mikopo.
C.3 — Mkopo wa Nje (Emergency Loan)
C.3a Endapo mfuko wa mikopo haukuwa na uwezo wa kutoa mkopo uliohitajika, kikundi kinaweza kujadili "mkopo wa nje" kutoka taasisi ya fedha au mwanachama mwingine — kwa uamuzi wa Bodi ya Uongozi na idhini ya Mkutano Mkuu.
C.4 — Riba ya Mikopo
C.4a Riba ya mkopo wa kawaida: 5% kwa mwezi wa kiasi kilichokopwa (flat rate). Riba inagawanywa kwa wanachama wote kama sehemu ya Gawio.
C.4b Riba haibadilishwi bila uamuzi wa Mkutano Mkuu kwa kura nyingi (simple majority). Mabadiliko ya riba yatatumika kwa mikopo MIPYA tu — si kwa mikopo iliyopo tayari.
SEHEMU D
Kanuni za Uongozi na Uchaguzi
5 Vifungu
D.1 — Katibu Msaidizi — Msemaji Mkuu wa Kikundi
D.1a Katibu Msaidizi ni Msemaji Mkuu rasmi wa kikundi kwa umma na vyombo vya habari, na pia Msimamizi Mkuu wa mfumo wa kidijitali (Admin). Yeye ndiye kiungo kati ya kikundi na ulimwengu wa nje.
D.1b Matangazo yote rasmi ya nje — iwe kwa WhatsApp wa umma, vyombo vya habari, au washirika wa biashara — lazima yapitie Katibu Msaidizi kwa idhini ya awali ya Mwenyekiti Mkuu.
D.2 — Maadili ya Kiongozi
D.2a Kiongozi HARUHUSIWI: (1) Kufanya maamuzi ya fedha ya zaidi ya TSh 50,000 peke yake bila kibali, (2) Kukusanya fedha kutoka kwa mwanachama yeyote bila utaratibu rasmi wa mfumo, (3) Kufanya mikataba kwa niaba ya kikundi bila idhini ya Bodi.
D.2b Kiongozi mwenye ukinzani wa maslahi katika jambo linalojadiliwa LAZIMA atangaze ukinzani huo wazi mbele ya kikao na atoke nje wakati wa mjadala na kupiga kura.
D.2c Kiongozi anayekiuka maadili haya atapewa onyo rasmi la kwanza. Kama ukiukaji utaendelea au kurudiwa, atafukuzwa mamlakani kwa kura ya dharura ya 2/3 ya wanachama wote hai.
D.2b — Kanuni ya Muda wa Uongozi
D.2b-1 Kiongozi anashikilia nafasi yake kwa miaka miwili (2) kamili. Baada ya kipindi kimoja cha miaka 2, LAZIMA apumzike kwa miaka 2 kamili kabla ya kugombea tena nafasi yoyote ya uongozi.
D.2b-2 Wakati wa kipindi cha pumziko, kiongozi wa zamani ANAWEZA: kutoa ushauri, kushiriki katika kamati, kupiga kura kama mwanachama wa kawaida. HARUHUSIWI: kugombea nafasi yoyote ya uongozi (Mkuu au Msaidizi).
D.2b-3 Kanuni hii inalenga kuzuia mkusanyiko wa nguvu na kuweka kikundi freshness ya uongozi daima.
D.3 — Kamati za Kikundi: Muda na Muundo
D.3a Kamati ya Uwekezaji na Mipango (Kudumu, miaka 2): Makamu Mwenyekiti, Mhasibu Mkuu, Katibu Mkuu, na wanachama 2 wa kawaida.
D.3b Kamati ya Mikopo (Kudumu, mwaka 1): Wanachama 3 wasio uongozi wanaochaguliwa na Mkutano Mkuu.
D.3c Kamati za Muda (kwa kazi maalum): Ukaguzi, Nidhamu, Matukio, Usajili, n.k. Hazidumu zaidi ya miezi 6 bila uamuzi mpya. Taarifa ya uundaji inatangazwa kwa wanachama wote ndani ya siku 7.
D.4 — Ngazi za Mfumo wa Kidijitali
D.4a Super Admin: uwezo wote wa mfumo — kuongeza/kuondoa wanachama, kubadilisha mipangilio ya msingi, kuona taarifa zote.
D.4b Kiongozi/Admin: kusimamia data ya wanachama, kupitisha miamala, kuona taarifa za fedha — kwa idhini ya Bodi.
D.4c Mwanachama: kuona taarifa zake mwenyewe tu — Hisa, mkopo, Gawio, historia ya miamala. HAWEZI kuona taarifa za wanachama wengine.
SEHEMU E
Kanuni za Vikao
2 Vifungu
E.1 — Aina za Vikao na Ratiba
E.1a Kikao cha Ripoti ya Mwezi: kila mwezi mwishoni mwa mwezi, mtandaoni, kwa muda wa saa 1. Ripoti za fedha, Hisa, malipo ya mikopo, taarifa nyingine za kawaida.
E.1b Kikao cha Robo Mhula: kila miezi 3, tathmini ya uwekezaji na malengo. Muda: saa 2-3. Mtandaoni au ana kwa ana.
E.1c Kikao cha Nusu Mhula: miezi 6 — mapitio makubwa ya fedha na mipango. Mwanachama aliye nje ya mkoa anaruhusiwa kushiriki mtandaoni.
E.1d Mkutano Mkuu (AGM): mwaka mmoja — ana kwa ana (lazima). Uchaguzi, taarifa ya mwaka, mabadiliko ya katiba. Mwanachama aliye nje ya mkoa anaruhusiwa kushiriki mtandaoni na kupiga kura.
E.1e Kikao cha Dharura (EGM): kinapohitajika — taarifa si chini ya SAA 4. Mambo ya dharura tu.
E.2 — Udhuru wa Kutokuhudhuria Kikao
E.2a Sababu zinazokubalika za kutokuhudhuria: ugonjwa (na uthibitisho wa daktari iwapo inawezekana), dharura ya familia, safari ya nje ya mkoa (na taarifa ya awali), au sababu nyingine inayokubalika na Katibu.
E.2b Taarifa ya kutokuhudhuria LAZIMA itolewe kwa Katibu KABLA ya kikao — si baadaye. Sababu inayotolewa baada ya kikao haizingatiiwi.
E.2c Mwanachama aliyepewa ruhusa ya kutokuhudhuria HATALIPA faini. Mwenye udhuru usioidhinishwa atalipa faini ya TSh 20,000 bila kujali sababu.
SEHEMU F
Uwekezaji, Makato, Migogoro na Kuvunja Kikundi
2 Vifungu
F — Kanuni za Uwekezaji
F.a Uwekezaji wowote wa kikundi lazima upitishwe na Kamati ya Uwekezaji na Mipango kwanza, kisha na Bodi ya Uongozi, na hatimaye kuidhinishwa na Mkutano Mkuu kwa kura ya simple majority (au 2/3 kwa uwekezaji mkubwa).
F.b Uwekezaji wa zaidi ya 30% ya mtaji wote wa kikundi unahitaji kura ya 2/3 ya wanachama WOTE katika Mkutano Mkuu ulioitishwa mahususi.
F.c Ripoti ya kila uwekezaji itatoka kwa wanachama wote kila robo mwaka — ikionyesha mapato, hasara, na maendeleo.
F.1 — Makato kwa Mwanachama Anayetoka
F.1a Mwanachama anayejiuzulu anapata: Hisa Huru zake (50% ya Hisa zake zote). ANAKATWA Hisa za Uwekezaji (50% ya Hisa zake) — zinabaki kwa kikundi.
F.1b Mwanachama aliyefukuzwa kwa kosa zito: Hisa Huru tu. Hisa za Uwekezaji zinakatwa kabisa.
F.1c Kifo: mrithi anapata HISA ZOTE (Huru + Uwekezaji) + Gawio lolote lililokusanyika. Hakuna makato kwa kifo.
F.1d Malipo ya stahiki za mwanachama anayetoka yatafanywa ndani ya siku 30 baada ya makubaliano yote kukamilika.

Umeridhika na misingi yetu?

Jiunge na SMART FRIENDS leo — anza kuweka akiba, kupata mikopo ya haki, na kukua kifedha pamoja nasi.

Jaza Fomu ya Kujiunga